Wednesday, January 25, 2017

Athari za magonjwa ya ngono kwa wasichana

Wasichana wengi wanaojihusisha na maswala ya ngono katika umri mdogo wanakabiliwa na ongezeko la uwezekano wa kupata saratani ya mlango wa mji wa mimba (cervical cancer). Shingo ya mlango wa mji wa mimba ambayo haijakomaa inapokutana na misukosuko ya ngono hudhoofika na kupoteza nguvu za kukabiliana na mashambulizi ya virus vya Human Papilloma – (HPV) ambao husababisha saratani hiyo mapema au baadaye sana.
Virusi hawa huambukiza kwa njia ya kujamiiana na wanaume hata kama mwanaume atakuwa amevaa kondomu wakati wa kufanya tendo la ngono na msichana. Saratani hii ni tatizo kubwa la kiafya linaloongoza kwa vifo vya wanawake vitokanavyo na ugonjwa wa saratani katika nchi zinazoendelea. Saratani hii kwa kawaida huwapata wanawake wengi ambao huanza kufanya tendo la kujamiiana katika umri mdogo, miaka michache baada ya kuvunja ungo.
Wasichana na wanawake wenye wapenzi wengi, au wenye wapenzi wa kiume ambao wana mtandao mkubwa wa wapenzi wengine wengi, huwa katika hatari kubwa ya kupata maambukizi ya virusi wanaosababisha ugonjwa wa saratani ya mlango wa kizazi.
Kwa bahati mbaya sana wasichana wengi hupata maambukizi ya virusi hawa kwa kufanya ngono kwa mara ya kwanza, hata kama ni mara moja tu. Tatizo jingine kuhusiana na maambukizi ya virusi hawa ni kwamba, msichana anaweza kuishi na virusi hawa bila habari kwa miaka 10 hadi 15 hivi ndipo madhara yake yanapojitokeza kwa wazi.
Tatizo jingine linalowakabili wasichana wadogo wanaoendekeza ngono ni ugumba wakati watakapo hitaji kuzaa. Magonjwa mengi ya ngono hushambulia mirija ya uzazi na kusababisha mirija hiyo izibe. Mirija ya uzazi inapoziba, hushindwa kupitisha mayai kwa ajili ya kutunga mimba pale msichana atakapohitaji kupata watoto hapo baadaye.
Magonjwa ya ngono kwa wasichana pia husababisha maumivu makali na kuugua hasa pale tumbo la chini linaposhambuliwa. Msichana hupata ugonjwa wa mwanamimba yaani uambukizo katika mji wa mimba na wakati mwingine katika njia ya mkojo. Hii pia huambatana na maumivu makali wakati wa kukojoa.
Magonjwa mengine katika kundi hili la magonjwa mengi mbalimbali, husababisha madhara makubwa na ya muda mrefu. Kaswende inaweza kusababisha ugonjwa wa moyo na akili hasa pale msichana anapochelewa kupata matibabu sahihi. Magonjwa haya pia yanaweza kukaa mwilini kwa muda mrefu bila kuonyesha dalili huku yakiendelea kudhuru afya ya msichana.

No comments:

Post a Comment