Ni kawaida kwako kwenda matembezi pamoja na mtu wa jinsia tofauti. Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?
Unavutiwa na mtu wa jinsia tofauti naye anavutiwa nawe pia. Mara
kadhaa kwa siku unamtumia ujumbe mfupi kwenye simu au unampigia simu.
Je, huo ni urafiki wa kimapenzi?
Kila mara mnapokuwa katika tafrija pamoja na marafiki, unatumia muda
mwingi pamoja na mtu yuleyule wa jinsia tofauti. Je, huo ni urafiki wa
kimapenzi?
Huenda
haikuwa vigumu kwako kujibu swali la kwanza. Lakini huenda ulisita
kidogo kabla ya kujibu la pili na la tatu. Urafiki wa kimapenzi ni nini hasa?
Urafiki
wa kimapenzi ni urafiki kati ya watu wawili wanaovutiana kimahaba na
unatia ndani shughuli yoyote ya kirafiki ambayo wanafanya pamoja.
Kwa hiyo, jibu la maswali yote matatu ni ndiyo. Iwe
kwa simu, uso kwa uso, mbele ya watu, au mahali pasipo na watu, ikiwa
wewe na rafiki yako wa jinsia tofauti mnaonyeshana mahaba na
mnawasiliana kwa ukawaida, basi huo ni urafiki wa kimapenzi.
Ni nini kusudi la kuanzisha urafiki wa kimapenzi?
Urafiki
wa kimapenzi unapaswa kuwa na kusudi lenye kuheshimika, yaani,
kumsaidia mwanamume na mwanamke kujua ikiwa wanaweza kufungua ndoa.
Labda
vijana wenzako hawauoni urafiki huo kuwa jambo zito. Pengine
wanafurahia tu kuwa na rafiki wa pekee wa jinsia tofauti bila kusudi
lolote la kufunga ndoa. Huenda hata wengine wao wanawaona rafiki hao
kuwa tuzo au pambo ambalo linawafanya waheshimiwe.
Hata
hivyo, mara nyingi urafiki huo usio na msingi mzuri haudumu. Msichana
mmoja anayeitwa Heather alisema hivi: “Vijana wengi ambao wanaanzisha
urafiki wa kimapenzi, wanauvunja baada ya juma moja au mawili. Wanaanza
kuwa na maoni ya kwamba urafiki huo ni wa muda tu, na maoni hayo
yanawatayarisha kwa talaka badala ya ndoa.”
Ni wazi kwamba unapoanzisha urafiki wa kimapenzi na mtu fulani, hisia zake zinahusika. Kwa hiyo hakikisha kwamba una nia nzuri.—Luka 6:31.
Ukianzisha
urafiki wa kimapenzi bila kusudi la kufunga ndoa, utakuwa kama mtoto
anayechezacheza na kitu cha kuchezea kisha anakiacha
Jiulize:
Je, ungependa mtu fulani achezee hisia zako kama vile mtoto
anavyochezacheza na kitu cha kuchezea kisha anakiacha? Basi usimchezee
mtu mwingine! Biblia inasema kwamba upendo “haujiendeshi bila adabu.”—1 Wakorintho 13:4, 5.
Msichana
anayeitwa Chelsea anasema hivi: “Wakati mwingine ninaona kwamba urafiki
wa kimapenzi unapaswa kuwa jambo la kujifurahisha tu, lakini haliwezi
kuwa jambo la kujifurahisha tu ikiwa mtu mmoja anauchukulia urafiki huo
kwa uzito naye yule mwingine anauona kuwa mchezo tu.”
Dokezo: Ili ujitayarishe kwa ajili ya kuanzisha urafiki wa kimapenzi na ndoa, soma 2 Petro 1:5-7
na uchague sifa moja ambayo unapaswa kufanyia kazi. Baada ya mwezi
mmoja, chunguza uone umejifunza kuihusu kwa kadiri gani na umeifanyia
kazi kwa kadiri gani.
Je, nina umri wa kutosha kuanzisha urafiki wa kimapenzi?
Unafikiri ni umri gani unaofaa kijana kuanzisha urafiki wa kimapenzi?
Sasa mwulize mmoja wa wazazi wako swali hilohilo.
Kuna
uwezekano mkubwa kwamba jibu lako limetofautiana na la mzazi wako. Au
labda majibu yanafanana! Huenda ukawa kati ya vijana wengi ambao kwa
hekima wanasubiri kuanzisha urafiki wa kimapenzi hadi watakapokuwa na
umri wa kutosha kujielewa vizuri zaidi.
Hivyo
ndivyo Danielle, mwenye umri wa miaka 17 alivyoamua kufanya. Anasema
hivi: “Nikifikiria jinsi nilivyohisi miaka miwili iliyopita, sifa ambazo
ningependa mtu ninayetaka kufunga ndoa naye awe nazo ni tofauti sana
ninapolinganisha na zile ninazoangalia sasa. Kwa kweli, hata sasa sioni
kama ninaweza kufanya uamuzi mzuri kuhusu hilo. Ninapohisi kwamba
nimetulia kwa miaka kadhaa bila kubadili-badili utu wangu, basi
nitafikiria kuanzisha urafiki wa kimapenzi.”
Kuna
sababu nyingine kwa nini kuna hekima kusubiri. Biblia inatumia maneno
“upeo wa ujana” kufafanua kipindi katika maisha ya mtu ambapo hisia za
ngono na za kimahaba huanza kuwa na nguvu sana. (1 Wakorintho 7:36)
Kuwa na uhusiano wa karibu na mtu mmoja tu wa jinsia tofauti unapokuwa
na umri huo kunaweza kuchochea tamaa hizo na kuongoza katika mwenendo
usiofaa.
Ni kweli huenda hilo lisiwe jambo zito kwa vijana wenzako. Huenda wengi wao wakawa na tamaa ya kufanya ngono. Lakini si lazima—wala hupaswi—kufikiri kama wao! (Waroma 12:2) Isitoshe, Biblia inatusihi ‘tuukimbie uasherati.’ (1 Wakorintho 6:18) Unaposubiri hadi upite upeo wa ujana, tunaweza ‘kuondolea mbali msiba.’—Mhubiri 11:10.
Kwa nini nisubiri kabla ya kuanzisha urafiki wa kimapenzi?
Kuwa
chini ya mkazo wa kuanzisha urafiki wa kimapenzi kabla ya kuwa tayari
ni kama kulazimishwa kufanya mtihani wa somo ambalo umeanza tu
kujifunza. Bila shaka, utahisi kwamba umeonewa! Unahitaji wakati wa
kujifunza somo hilo ili uwe na habari zitakazokuwezesha kupita mtihani
huo.
Ndivyo ilivyo pia kuhusiana na urafiki wa kimapenzi.
Urafiki
wa kimapenzi si mchezo. Kwa hiyo, kabla ya kuwa tayari kumkazia fikira
mtu mmoja hususa, unahitaji kujifunza “somo” muhimu—jinsi ya kujenga
urafiki.
Baadaye,
utakapompata mtu anayekufaa, utakuwa tayari kujenga urafiki wenye
kudumu. Kusema kweli, ndoa nzuri ni muungano wa marafiki wawili wakubwa.
Kungoja muda upite kabla ya kuanzisha urafiki wa kimapenzi hakukunyimi uhuru. Badala yake, kunakupa uhuru zaidi wa ‘kushangilia katika ujana wako.’ (Mhubiri 11:9) Nawe utakuwa na wakati wa kujitayarisha kwa kuboresha utu wako, na zaidi ya yote, hali yako ya kiroho.—Maombolezo 3:27.
Kwa sasa, unaweza kufurahia
kushirikiana na watu wa jinsia tofauti. Jinsi gani? Njia bora ni
kushirikiana nao mkiwa katika vikundi vyenye mchanganyiko wa wavulana na
wasichana ambavyo vinasimamiwa vizuri. Msichana anayeitwa Tammy
anasema: “Nafikiri inafurahisha zaidi mambo yanapofanywa kwa njia hiyo.
Ni afadhali kuwa na marafiki wengi.” Monica anakubaliana naye. Anasema:
“Kushirikiana katika vikundi ni wazo zuri, kwa sababu unapata
kuchangamana na watu wenye nyutu tofauti-tofauti.”
Kwa
upande mwingine, ukimkazia fikira mtu mmoja tu mapema sana maishani,
huenda ukavunjwa moyo. Kwa hiyo, usiwe na haraka. Tumia wakati huu wa
maisha yako kujifunza jinsi ya kusitawisha na kudumisha urafiki.
Baadaye, ukichagua kuanzisha urafiki wa kimapenzi, utakuwa umejifahamu
vizuri zaidi na kufahamu sifa ambazo ungependa mwenzi wa ndoa awe nazo.
No comments:
Post a Comment